Na:George Binagi-GB Pazzo @BMG
Chama
cha Demokrasia na Maendeleo Chadema kimesitisha shughuli za mazishi ya
aliekuwa Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoani Geita marehemu Alphonce
Mawazo, baada ya jeshi la polisi Mkoani Mwanza kuzuia zoezi la kuuaga
mwili wake lililokuwa limepangwa kufanyika juzi jumamosi Jijini Mwanza.
Mwenyekiti
wa Chama hicho Taifa, Freeman Mbowe alibainisha hayo jana wakati
akizungumza na Wanahabari Mkoani Mwanza, ili kutoa msimamo wa Chama
baada ya kuwepo kwa mazungumzo baina yake na familia ya marehemu
Mawazo.
Alisema
kuwa baada ya mazungumzo hayo, Chadema pamoja na familia ya marehemu
Mawazo wamekubaliana kwenda Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza kufungua shauri
la kuomba tafsiri ya Kimahakama juu ya zuio hilo la jeshi la polisi
kuzuia mwili wa marehemu Mawazo kuagwa Jijini Mwanza kabla ya Kwenda
kuzikwa Kijijini kwake Chikobe katika Wilaya ya Busanda Mkoani Geita.
Nae
Mchungaji Charles Lugiko ambae ni baba mlezi wa marehemu Mawazo,
alisema anasikitishwa na hatua iliyochukuliwa na jeshi la polisi ya
kuzuia mwili wa marehemu Mawazo kuagwa Jijini Mwanza ambapo ameeleza
kuwa na matumaini makubwa ya kwamba mahakama itatenda haki juu ya suala
hilo.
Frederick
Sumaye pamoja na Edward Lowasa ambao ni Viongozi Waandamizi wa Chadema,
walisema hatua ya jeshi la polisi kuzuia mwili wa Mawazo kuagwa Jijini
Mwanza si sawa na kwamba inaweza kuwa chanzo cha uvunjifu wa amani.