Nawasalimuni
nyote katika jina la nchi yetu nzuri Tanzania,
Jina ambalo huko nyuma sote tuliliimba “Tazama ramani utaona nchi nzuri,
yenye mito na mabonde mengi ya nafaka…nchi hiyo mashuhuri huitwa
Tanzaniaaa!”
Hakika wimbo huu vijana wengi siku hizi wanashindwa kuuimba, kwa nini?
Uzuri wa taifa lao haupo tena, umepotezwa na baadhi yenu watumishi wa
umma
wasio na uadilifu.
Sio
siri vijana wetu kwa muda mrefu wameshindwa kujivunia taifa lao,
wameshindwa kuongea mbele za watu kwa sauti kubwa kwamba wao ni
Watanzania,
uzuri wa taifa lao na sifa nzuri ya nchi yao imeharibiwa na vitendo kama
ufisadi uliokithiri ambao umesababisha wachache katika taifa kunufaika
huku wengi
wakiteseka.
Ndugu zangu watumishi wa umma,
Ni kwa kupitia jina la nchi hii ndiyo leo nawaandikieni, kuwakumbusha
juu ya wajibu wenu ambao kwa muda mrefu sana umekuwa hautimizwi
ipasavyo!
Kwanza
kabisa niseme wazi kwamba nayafahamu mateso yenu, nayafahamu mahangaiko
yenu ya maisha magumu, ambayo wakati mwingine yamefanya
uaminifu wenu kutikiswa.
Pamoja na hayo yote nasema hakuna jambo hata moja linalohalalisha kwenu
ninyi kupoteza vigezo vitano muhimu vya utumishi wa umma ambavyo ni;
1.UADILIFU
2.UAMINIFU
3.KUSEMA KWELI DAIMA
4.UZALENDO NA DHAMIRA
5.HOFU YA MUNGU.
Yeyote
kati yenu aliyehalalisha kuondoka kwa vitu vitano nilivyovitaja hapo
juu kwa sababu ya aidha kipato kidogo anachokipata serikalini,
akavunjika moyo na
kuacha kuwatumikia wananchi, ama akachagua kuendeleza rushwa na kukosa
uzalendo, huyu hatufai kuwa mtumishi wa umma. Kwa muda mrefu mmekuwa
mkilalamikiwa, mkinung’unikiwa na wananchi kwa sababu ya utendaji mbovu
unaosababishwa na kukosekana kwa mambo matano niliyoyataja hapo juu,
kwa kweli ilionekana kana kwamba uadilifu katika taifa hili hauwezekani
tena, vivyo hivyo uaminifu, kusema kweli, uzalendo na hofu ya Mungu
vilitoweka.